Skip to main content

MIKATABA YA LUGHA ZA KIGENI KWA WANANCHI YAMKERA NAIBU WAZIRI.

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew (wa tatu Kulia
mstari wa mbele) akifuatiwa na Mbunge wa Muheza Mhe. Hamis Mwinjuma wakisikiliza maelezo
ya Mradi wa Ujenzi wa mnara wa mawasiliano kutoka kwa mwakilishi wa kampuni ya Halotel
(mwenye shati la pinki) wakiwa eneo la mradi wa ujenzi wa mnara wa mawasiliano wa kampuni
hiyo wengine ni wananchi na baadhi ya watendaji wa Serikali walioambatana nae.


Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew akizungumza na
watendaji wa TTCL kuhusu usambazaji wa huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano katika
chumba cha maunganisho ya huduma hiyo kilichopo katika jengo la Mamlaka ya Mapato
Tanzania (TRA) Horohoro Wilayani Mkinga.



Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew (kushoto)
akizungumza na watendaji wa TRA katika eneo la mashine ya kukagulia mizigo alipotembelea
jengo hilo kwa lengo la kukagua huduma ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano iliyofikishwa
katika jengo la hilo la TRA na Ofisi mbili za Serikali za TRA na Uhamiaji zilizopo katika jengo hilo
kuunganishiwa huduma hiyo.


Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew (kushoto) alipowasili katika Ofisi za TRA na Uhamiaji zilizopo katika Mpaka wa Horohoro Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga kukagua huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano na mwingiliano wa Mawasiliano mipakani. Anayefuatia ni Kanali Maulid Surumbu Mkuu wa Wilaya ya Mkinga.

Na Mwandishi wetu, MUHEZA

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Mhandisi Kundo Mathew amesikitishwa na tabia ya baadhi ya watendaji wa makampuni ya simu nchini kuwasainisha wananchi mikataba au makubaliano yeyote ya kutumia ardhi ya mwananchi kujenga mnara kwa lugha za kigeni

Akiwa katika ziara yake ya kukagua ujenzi, uwezo na ubora wa minara ya mawasiliano katika Wilaya ya Muheza Mkoani Tanga Mhandisi Kundo alitembelea mradi wa ujenzi wa mnara wa Haloteli uliopo katika Kijiji cha Tanga B ambapo baada ya kumhoji mmiliki wa eneo hilo alisema kuwa alisaini mkataba wa makubaliano ya awali ya kufanya ujenzi katika eneo lake uliokuwa kwa lugha ya Kiingereza na kivietinamu.

Mhandisi Kundo amepiga marufuku kumsainisha mwananchi mkataba kwa lugha za kigeni kwasababu yeyote anayefanya hivyo lazima kutakuwa na dhamira ovu dhidi ya mwananchi ndio maana anasainishwa mkataba kwa lugha asiyo ifahamu.

Aliongeza kuwa, Serikali itasimamia haki na maslahi ya wananchi kwa kuhakikisha wanasainishwa mikataba kwa lugha ya Kiswahili na kiingereza ili pande zote ziweze kunufaika kwa mwananchi kusaini kitu anachokielewa na kulipwa fedha kulingana na ukubwa wa maeneo wanayoyatoa kwa ajili ya ujenzi wa minara ya mawasiliano.

Amesema kuwa dhamira ya Wizara hiyo ni kuondoa migogoro ndani ya Sekta ya Mawasiliano kwa watoa huduma kufuata taratibu wakati wa ujenzi wa minara ikiwa ni pamoja na kupata vibali vinavyohitajika na kusaini mikataba na Serikali za vijiji kwa ajili ya ulinzi wa minara ya mawasiliano

Aidha, Mhandisi Kundo alitoa maagizo kwa watoa huduma kufanya malipo kupitia akaunti za benki kutoka kwenye kampuni kwenda moja kwa moja kwa walioingia nao mkataba ambao ni wamiliki wa maeneo waliyojenga minara ili kampuni kujiridhisha inamlipa mhusika na sio vinginevyo

Wananchi wa Kijiji cha Tanga B kilichopo katika Kata ya Kwabada Wilayani Muheza walikiri mbele ya Naibu Waziri huyo kuwa wanahitaji mnara huo wa kampuni ya Halotel ujengwe kwa ajili ya kuwapatia mawasiliano baada ya kampuni hiyo kuhakikisha imefuata taratibu za kupata vibali vinavyohitajika

Kabla ya kufika katika Kijiji hicho Mhandisi Kundo alifanya ziara katika mpaka wa Horohoro uliopo katika Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga ambapo alikagua Kituo cha Huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano pamoja na kukagua Jengo la TRA lililounganishwa na huduma za Mkongo huo pamoja na kukagua mwingiliano wa mawasiliano na nchi jirani ya Kenya ambapo iligundulika kuwa Kampuni ya simu ya Vodacom imefanikiwa kuzuia muingiliano wa mawasiliano katika mpaka huo ili kudhibiti mwingiliano wa mawasiliano katika maeneo ya mipaka, Mhandisi Kundo alielekeza taasisi mbili za mawasiliano ambazo ni Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania

(TCRA) na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kuhakikisha wanakuja na majibu ya kupaa suluhisho la kudumu tatizo la muingiliano wa mawasiliano katika maeneo yote ya mipaka nchini ifikapo tarehe 16 AQgosti,2021.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Comments

Popular posts from this blog

Mkuu wa Mkoa wa Katavi akibidhiwa Ofisi,aelezwa Miradi ya kusimamia.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Bi,Mwanamvua Hoza Mrindoko wa kwanza Kushoto akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Zuberi Homera wakati wa makabidhiano ya Ofisi. Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Katavi Beda Katani. Wakuu wa Wilaya,Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Jamila Yusuf na Mkuu wa Wilaya ya Mlele Rachel Kasanda. Na Mwandishi Wetu,Site Tv Mapema leo Mei 25,2021 Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Hoza Mrindoko,amekabidhiwa Ofisi na aliye kuwa Mkuu wa Mkoa huo Juma Zuberi Homera aliye hamishiwa Mkoani Mbeya kuwa Mkuu wa Mkoa. Katika makabidhiano hayo,Homera amemtajia Mkuu wa Mkoa wa Katavi miradi ambayo inatakiwa kusimamiwa hadi ikamilike ni pamoja na Bandari ya Karema,Hosipitali ya Rufaa Mkoa,Kiwanda cha Nguo,Jengo la Utawala pamoja na Umeme wa Gridi ya Taifa. Aidha,amesema Katavi ni Nyumbani hivyo atatoa ushirikiano kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi huku akiwakaribisha Viongozi na Wananchi kwa ujumla katika Mkoa wa Mbeya. "Kuna hili la Gridi ya Taifa ambalo linaendelea,kuna Kiwan...

Tabasamu hili kwa Wanafunzi,Nuru imewaka Juu yao/Mwekezaji afanya Jambo ...

Ajira Mpya Wakaribishwa Mlele, Full Kula Bata/Makubwa yaja