Na Swaum Katambo
Tanganyika-Katavi
Wafugaji wa Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi wameonywa tabia ya kutumia vibaya majina ya viongozi ili kujificha katika kichaka cha uharibifu wanaofanya wa kupeleka mifugo katika mashamba ya wakulima na kuharibu mazao.
Hatua hiyo inakuja mara baada ya wakulima wa Kijiji cha Majalila kulalamika na kuhoji kwa Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Salehe Mhando juu ya kero ya majibu mabaya wanayoyapata kutoka kwa wafugaji pindi wanapo wakamata wafugaji wakilisha mifugo yao kwenye mazao na kujibiwa "Hata mfanye nini hamna pa kutupeleka kwanza mifugo hii ni ya Mkuu wa Wilaya".
Ili kuondoa Mgogoro huo baina ya Wakulima na Wafugaji DC Mhando amewaagiza Mtendaji wa Kijiji na Mtendaji wa Kata kuwatambua kwa majina wafugaji wote waliopo Tanganyika pamoja na mifugo yao ili kuwapangia maeneo ya vitalu kwa ajili ya kulisha mifugo yao.
Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Salehe Mhando akizungumza na wakulima wa wa Kijiji cha Majalila.
Katika hatua nyingine wakulima wa Vitongoji vya Ijenje na Masemba Wilayani Tanganyika wametoa Gunia 2 za Maharage,Debe moja la Mchele na Kuku kama ishara ya shukrani kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Salehe Mhando kwa kitendo cha kuwapigania na kusimamia kurudishiwa mashamba yao ambayo yalitwaliwa na Idara ya Misitu (TFS) Mpanda.
"Mnamo tar 29/07/2017 wananchi wa Kampemba tulikumbwa na matatizo makubwa ya kupuuzwa, kunyanyaswa, kudharauliwa na hatimaye kufukuzwa na kuporwa mali zetu na kuchomewa majumba na Idara ya Misitu (TFS) Mpanda".Alisema Amisa Ramadhani Mng'omba wakati akisoma Risala kwa niaba ya wakulima wenzake mbele ya DC Mhando.
Kufuatia kadhia hiyo wakulima hao wamesema waliathirika kisaikolojia, waliibiwa mamilioni ya fedha, walikosa mahali pa kuishi na pia kukosa mashamba na kusema kuwa kitendo hicho kiliwasababishia kukosa chakula kabisa kwani waliacha mashamba yao ya nafaka yakiharibika hivyo nyani, wezi pia kuungua na moto, na hatimaye Kaya hizo zilikumbwa na njaa kwa kipindi cha miaka minne(4).
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Salehe Mhando alitoa shukrani kwa niaba ya Kamati ya Ulinzi na Usalama kwa kazi ambayo wamekuwa wakishirikiana na Wakulima kuhakikisha kwamba wanafanya shughuli zao bila bugudha yoyote huku akitumia fursa hiyo kutoa Motisha kwa kumkabidhi Bati 32 Mwenyekiti mstaafu wa Kijiji cha Majalila Noely Kalikiti huku akitarajia pia kutoa Motisha kwa wenyeviti wastaafu wa Vijiji vya Kibo na Lugonesi.
Baadhi ya wakulima wa wa Kijiji cha Majalila wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Salehe Mhando.
Comments
Post a Comment